Bwawa la maji machafu katika mgodi wa Williamson Diamond wa mkoani Shinyanga, limepasuka na tope kutiririka kwenye makazi ya watu na kusababisha nyumba 13 kuzingirwa na tope na maji machafu huku wakazi wakilazimika kuyahama makazi yao kwa muda kwa ajili ya usalama.
Ni wakazi wa vijiji vya Mwangolo na Nyenze, Kata ya Mwaduiluhumbo ambao wameiomba serikali kuwapa msaada wa haraka kutokana na nyumba zao kuzungukwa na tope lililotokana na bwawa la kuhifadhi maji machafu katika mgodi wa Williamson kupasuka na kutiririka kwenda kwenye makazi ya watu na kwenye mashamba
Akitoa ufafanuzi wa tukio hilo Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Sophia Mjema, amesema katika uchunguzi wa awali wamebaini nyumba 13 zimezungukwa na maji machafu pamoja na tope na tayari ameunda tume ili kujua kama kuna athari zaidi na chanzo cha bwawa hilo kupasuka.