WATU wanaokadiriwa kufikia 1,920 kutoka kaya 320 na ofisi za serikali katika Kata ya Kitanda mwambao mwa Ziwa Tanganyika hawana makazi baada ya kuzikimbia nyumba zao ambazo zimezingirwa na kujaa maji.
Hali hiyo imetokana na Ziwa Tanganyika kuendelea kujaa maji.
Diwani wa Kata ya Kirando, Kakuli Seba akizungumza na HabariLEO katika mahojiano yaliyofanyika kando ya kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kilichofanyika mwishoni mwa wiki katika mji mdogo wa Namanyere.
"Nyumba 320 ambazo ni za kisasa zimezingirwa na kujaa maji katika vijiji vya Mtakuja na Kichangani na kusababisha wananchi kuzikimbia nyumba zao na vyumba vya kupangisha kupanda bei kutoka Sh 10,000 hadi Sh 30,000 kwa mwezi kwa chumba kimoja kisichokuwa na maji...baadhi yao wamejihifadhi kwa majirani huku wachache wenye uwezo wamepanga vyumba" alifafanua na kuongeza:
"Kila upepo wa Kaskazi unapovuka, ujazo wa maji ziwani unaongezeka na kusababisha mafuriko,"alieleza.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi, Nissan Kwangura alisema tayari viwanja vya makazi vimetengwa na kupimwa jirani na eneo la Shule ya Sekondari Nkasi ili vigawiwe kwa waathirika wa mafuriko ya maji ya Ziwa Tanganyika.