Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Amos Makalla @amosmakalla ameagiza kufunguliwa kwa Baa na Hoteli zote zilizofungiwa na Baraza la Taifa la Mazingira (NEMC) kwa kosa la kufungulia muziki mkubwa na kuweka utaratibu wa haraka wa kuelimisha makundi hayo.
“Baa na Hotel hizi zikisimama ajira zitasimama, biashara zitasimama na uchumi utasimama na tujiulize watawezaje kulipa faini wanazodaiwa wakati biashara wamefunga hawafanyi tena”
Makalla pia amepiga marufuku ukamataji wa nguvu huku akisema kuwa Wafanyabiashara hao sio majambazi hivyo wanapaswa kuelimishwa wanapokosea kwa kuangalia uhalisia wa maisha kwani kuua biashara ni rahisi sana kuliko kuijenga.
Ameitaka NEMC na Wafanyabiashara waliopigwa faini kuketi pamoja na kuzungumza namna ya kumaliza matatizo hayo ili kuhakikisha biashara hazisimami kwa sasa na amewataka watulie na kuondoa hofu kutokana na tafrani za kamatakamata.