Mwanza. Makaburi ya waliofariki dunia katika ajali ya Mv Bukoba yaliyoko Igoma jijini Mwanza yako hatarini kufukuliwa na mafuriko kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha baada ya uzio uliojengwa kuyazunguka kuangushwa na maji.
Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi juzi katika eneo hilo lenye makaburi zaidi ya 400 umegundua kuwa baadhi ya makaburi tayari yameanza kudidimia kutokana na wingi wa maji ya mvua yanayoingia eneo hilo.
Ajali ya Mv Bukoba ilitokea Mei 21, 1996 na kusababisha vifo zaidi ya watu 1,000 ambao baadhi yao walizikwa kwenye makaburi ya pamoja eneo la Igoma Barabara Kuu ya Mwanza – Musoma, nje kidogo ya jiji la Mwanza.
Akizungumzia suala hilo, mmoja wa majirani wanaoishi eneo hilo, Deus Ndaki aliiomba Serikali kupitia Halmashauri ya Jiji la Mwanza kujenga upya uzio ulioanguka kulinda hadhi ya Watanzania waliopumzishwa kwenye makaburi hayo.
“Hii ni sehemu ya kumbukumbu muhimu kitaifa. Ni lazima patunzwe kwa heshima ya waliolala hapo,” alisema Ndaki.
Mkazi mwingine, Emmanauel Machumu alisema ni jambo la aibu ukuta wa makaburi hayo kuanguka na kuachwa muda mrefu bila kurekebishwa upya.
Pia Soma
- VIDEO: Maji ya ziwa Victoria yavunja rekodi
- VIDEO: Salamu za Magufuli kwa familia ya aliyekuwa Katibu mkuu wa CUF, Khalifa Suleiman
- Walimu wasaka wanafunzi Ufaransa
Akizungumzia suala hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Kiomonio Kibamba alisema ofisi yake tayari imemwagiza mhandisi wa jiji kufanya tathmini kujua gharama za kujenga upya ukuta huo.
“Tunayathamini na kuyaheshimu makaburi ya waliofariki dunia katika ajali ya Mv Bukoba kwa sababu ni eneo la kumbukumbu la kitaifa. Tutajenga upya ukuta uliodondoka na tayari tathmini inafanyika,” alisema Kibamba.