Dar es Salaam. Idadi ya waliokufa kutokana na ajali ya moto iliyotokea mkoani Morogoro imefikia 104 baada ya majeruhi wawili kati ya 13 waliokuwa wamelazwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dar es Salaam kufariki dunia.
Ajali hiyo ilitokea Agosti 10, 2019 katika mtaa wa Itingi, Msamvu barabara ya Morogoro-Dar es Salaam baada ya lori la mafuta ya petroli kupinduka na kuwaka moto muda mfupi baada ya watu kuanza kuchota mafuta.
Akizungumza leo Jumapili Septemba 1, 2019, mkuu wa kitengo cha mawasiliano wa MNH, Aminiel Aligaesha amesema Asha Ally Seleman (28) alifariki Jumatano iliyopita ya Agosti 28, 2019 na Avelina Pastory Aman (30) alifariki jana Jumamosi Agosti 31,2019.
Amesema majeruhi 11 ndio wamebaki hospitalini hapo kati ya 47 waliopokelewa tangu ajali hiyo ilipotokea ambapo 36 wamefariki.
Aligaesha amesema kati ya majeruhi 11 wanaoendelea kutibia MNH sita wapo wodi 22 ya Sewahaji na watano wako Chumba cha ungalizi maalum (ICU).
Majeruhi wengine 16 wanaendelea na matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.
Habari zinazohusiana na hii
- VIDEO: Madaktari wataja sababu vifo zaidi ajali ya moto Morogoro
- VIDEO: Watu zaidi ya 57 wafariki dunia baada ya lori la mafuta kulipuka Morogoro
- Waliofariki ajali ya moto Morogoro wafikia 95
- Mmoja afariki dunia ajali nyingine ya lori la mafuta kuteketea kwa moto nchini Tanzania