Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Majaliwa mgeni rasmi miaka 60 Zinjanthropus

66865 Pic+zinja

Mon, 15 Jul 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Arusha. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassimu Majaliwa anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika kilele cha maadhimisho ya kumbukumbu ya kugunduliwa fuvu la Zinjanthropus Julai 22 mwaka 2019, katika makumbusho ya Olduvai, ndani ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA).

Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya maadhimisho hayo, Profesa Audax Mabula akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Julai 15,2019 amesema Majaliwa anatarajiwa pia kuzindua makumbusho ya watafiti waliogundua fuvu hilo, Julai 17 mwaka 1959, Dk Louis Leakey na mkewe Dk Mary Leakey.

Amesema makumbusho ya watafiti hayo, ambayo yametunzwa na Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro, kuna vifaa mbalimbali walivyokuwa wakitumia, nyumba waliokuwa wanalala, gari waliyokuwa wanatumia.

"Haya ni makumbusho ya kihistoria duniani katika masuala ya utafiti wa kujua chimbuko la binaadamu na hadi sasa eneo la Olduvai ndilo linatambulika ni moja ya maeneo duniani ambayo watu wa kale na wanyama wa aina mbalimbali waliishi," amesema

Profesa Mabula amesema kauli mbiu ya maadhimisho hayo ni tujivunie  urithi na chimbuko letu, ambapo watafiti kutoka maeneo mbalimbali duniani, watalii wa ndani na nje watapata fursa ya kutembelea makumbusho  na maonesho ya urithi wa tamaduni.

Meneja Idara ya Urithi wa Utamaduni wa Mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro, Joshua Mwaikunda amesema  wameandaa ofa ya kutembelea makumbusho ya Olduvai katika maadhimisho hayo ambayo yataanza Jumatano ya Julai 17,2019  yakiambatana na warsha ya watafiti kutoka maeneo mbali mbali duniani.

Pia Soma

Anasema gharama za kutembelea makumbusho na maonesho Ngorongoro ni Sh30,000 kwa watu wazima na watoto Sh15,000 na fedha hizo ni gharama ya usafiri kutoka Karatu na chakula.

"Kunakuwa na maonesho ya maeneo yote ya kale, ikiwepo Kondoa Irangi, makumbusho ya taifa na maeneo mbalimbali nchini yenye urithi wa utamaduni," amesema

Meneja uhusiano wa NCAA, Joyce Mgaya ametoa wito kwa Watanzania na wageni kutembelea makumbusho ya Olduvai  kujionea historia  ya binaadamu ambayo haipatikani sehemu yoyote duniani.

"Hii ni fursa ya kipekee kwa watanzania ma watafiti duniani kukutana Olduvai kujifunza mambo kale na kujionea urithi wa utamaduni uliopo nchini," amesema.

Chanzo: mwananchi.co.tz