Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa leo amekagua kitalu cha miche ya mkonge cha TARI Mlingano kilichopo wilayani Muheza, Tanga na kufungua zoezi la ugawaji wa miche kwa wakulima wa zao hilo.
Akizungumza wakati wa tukio hilo Majaliwa ameziagiza halmashauri zinazolima mkonge nchini pamoja na wakulima wakubwa wa wa zao hilo watenge ekari 10 kwa ajili ya kuanzisha vitalu vya kuzalisha miche ya mkonge ili kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wake.
Aidha, Majaliwa ameiagiza Wizara ya Kilimo itenge fedha katika bajeti yake kwa ajili ya kituo cha TARI Mlingano ili kukiwezesha kupanua eneo la uzalishaji miche kwa kununua vitendea kazi yakiwemo matrekta.
Amesema kituo cha TARI Mlingano kinatakiwa kijikite katika kufanya utafiti wa mbegu bora pamoja na dawa za kudhibiti magonjwa katika zao hilo na suala la uzalishaji wa mbegu lifanywe kwa ushirikiano katika ya kituo hicho na wadau wa zao hilo.