Bariadi. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majliwa amewasili katika viwanja vya Nyakabindi wilayani Bariadi katika hafla ya kuhitimisha maonyesho ya Nanenane kitaifa.
Katika hafla hiyo Majaliwa amemuwakilisha Rais wa Tanzania, John Magufuli aliyetarajiwa kuwa mgeni rasmi lakini hajaweza kufika kutokana na mkutano Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika(SADC) inayoendelea jijini Dar es Salaam.
Maonesho hayo yanayofanyika Nyakabindi kwa mwaka wa pili mfululizo yana zaidi ya zaidi ya washiriki 300 kutoka wizara mbalimbali, halmashauri, mashirika, taasisi za umma, kampuni na watu binafsi.
Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini amesema Majaliwa atashuhudia shughuli ya ununuzi na usombaji wa pamba kupitia malori yaliyosheheni marobota ya pamba yaliyoegeshwa pembezoni mwa jukwaa kuu la mikutano.
Waziri Mkuu pia atakabidhi zawadi, ngao na vyeti kwa washindi mbalimbali waliofanya vema katika uoneshaji wa bidhaa na huduma.
Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka amewaomba wakazi wa Bariadi na wilaya jirani kujitokeza kwa wingi kuhudhuria kilele cha maonesho hayo kujifunza mbinu bora za kilimo, ufugaji na uvuvi.
Pia Soma
- Bosi TBS awasimamisha kazi watumishi wawili kituo cha Namanga
- UCHOKOZI WA EDO: Pambano la Waraka na ‘Clip’ limeisha sare?
- Wafanyabiashara 12 wadakwa wakidaiwa kubadilisha fedha bila kuwa na kibali