Mwanza. Mwili wa aliyekuwa Rais wa tano Tanzania, Hayati John Magufuli aliyefariki dunia kwa ugonjwa wa moyo Machi 17, 2021 leo Jumatano Machi 24, 2021 utapitishwa katika daraja la JPM eneo la Kigongo-Busisi ambalo ujenzi wake unaendelea.
Daraja hilo lenye urefu wa kilomita 3.2 na refu kuliko yote katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na ni kati ya miradi mikubwa ya sekta ya ujenzi wa miundombinu aliyoianzisha na kiongozi huyo.
Uamuzi wa kupitisha jeneza lenye mwili wa Magufuli juu ya daraja hilo lililopewa jina lake kama ishara ya heshima na kutambua mchango wake katika ulitangazwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipokuwa Zanzibar jana Jumanne Machi 23, 2021.
Litakapokamilika daraja la JPM linalopita katika Ziwa Victoria na kuunganisha Wilaya za Misungwi na Sengerema siyo tu litawezesha watu kutumia dakika nne kuvuka eneo hilo kulinganisha na muda wa kati ya dakika 40 hadi saa nzima, bali pia utaokoa maisha ya wagonjwa wanaofariki dunia wakisubiri kivuko.
Daraja hilo pia litarahisisha usafirishaji na kusisimua biashara kati ya mikoa ya Kanda ya Ziwa ya Mwanza, Geita, Kagera, Kigoma na nchi jirani za Uganda, Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).