Lindi. Rais wa Tanzania, John Magufuli amewataka watendaji wa serikali waliojilipa fedha kiasi cha Sh49 milioni zilizokuwa za ukarabati wa wodi ya watoto katika hospitali ya mkoa ya Sokoine mkoani Lindi kuzirudisha mara moja.
Rais Magufuli ametoa maagizo hayo leo Jumanne, Oktoba 15, 2019 wakati akizungumza na wananchi wa kijiji cha Kiwalala jimbo la Mtama wakati akienda Wilaya ya Ruangwa kwa ziara.
Ameanza kwa kuwashukuru wananchi kwa kumpa kura na kusema Serikali imekuwa ikiendelea kutatua kero za wananchi lakini baadhi ya fedha za miradi zimekuwa zikitumika vibaya kwa watumishi kujilipa na kuwataka wakurugenzi wa halmashauri na wakuu wa wilaya kuzisimamia.
“Pamekuwa na mchezo mmoja katika hospitali moja iliyojengwa watu wakawa wanajilipa watumishi, hospitali ya mkoa Sokoine kuna upotevu wa Sh89 milioni zilizolipwa NHIF, kuna kuuzwa gari ya aina ya Land Cruiser wakati gari ni nzima na hospitali haina gari,” amesema Rais Magufuli
“Matumizi mabaya ya fedha za ukarabati wodi ya watoto, mfano watendaji kutumia Sh49 milioni kujilipa na wako hapa hapa.”
“Nataka watendaji wote waliojilipa hizo fedha wazirudishe, nimeona niyazungumze haya mapema ili hospitali ya wilaya Mtama watendaji wasije wakaenda kujilipa, fedha yote Sh1.5 bilioni ni kwa ajili ya kujenga hospitali,” amesema Rais Magufuli
Pia Soma
- Magufuli aagiza Halmashauri Lindi Vijijini iitwe Mtama, atoa siku 15 kwa DED, DC
- Mbowe: Hatutasusa uchaguzi, hatutokubali kuchakachuliwa matokeo
- Mbowe atoa kauli uandikishaji wapiga kura