Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Omary Mgumba amewaasa madereva wa Tanzania na nchi jirani wanaotumia mpaka wa Tunduma kupuuza ujumbe unaosambaa kwenye mitandao ya kijamii kuwataka wagome siku ya Jumamosi Septemba 4, 2021.
Wito huo umetolewa Alhamisi Septemba 2, 2021 wakati Mkuu huyo wa Mkoa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake amesema kuna watu ambao wanajitambulisha kama madereva wanawahamasisha wenzao kugoma siku hiyo.
"Kutokana na ujumbe unaoendelea kusambaa, nikubali kuwa madai ya madereva yana ukweli kwani viongozi walishafika ofisini kwangu kuwasilisha malalamiko yao na baadhi tayari serikali imeanza kuyafanyia kazi na kuyapatia ufumbuzi," amesema Mgumba
RC Mgumba amesema kati ya hoja zilizowasilishwa kwake, zipo hoja za ndani ya nchi nyingine zinazotokana na nchi jirani hasa madereva wa Tanzania wanapokuwa kwenye nchi hizo ambazo zinahitaji utatuzi wa kidiplomasia kwa panda zote kukutana.
Ametaja baadhi ya malalamiko ya madereva kuwa ni pamoja na kulazimishwa kuegesha magari kwenye maegesho ya kulipia hata kama muda unaruhusu kuendelea na safari, sheria mpya inayowataka madereva hao kutakiwa kutoingia nchini Zambia na badala yake kuachia madereva wazambia waendeshe hali ambayo inatishia ajira zao.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa mawakala wa kusafirisha magari nje ya nchi Waziri Msangi amekiri kuwepo na mgomo siku ya Jumamosi Kutokana na madai yao mbalimbali kutopatiwa ufumbuzi.