Moshi. Baada ya kumalizika kwa mgomo wa daladala mjini Moshi uliodumu kwa takriban siku nne, baadhi ya madereva wa Bajaj mjini hapa wamesitisha kutoa huduma ya usafiri kwa madai ya kukamatwa na mgambo na kutozwa faini.
Wametangaza mgomo huo leo Jumatano Desemba 12, 2018 baada ya wenzao wanane kukamatwa kwa tuhuma za kuegesha Bajaj na kupakia abiria maeneo yasiyo rasmi.
Wiki iliyopita daladala zinazofanya safari zake katika maeneo kadhaa ya mji huo, zilisitisha kutoa huduma ya usafiri kwa madai ya Bajaj kupakia abiria katika vituo vya mabasi.
Katibu wa Umoja wa Bajaj Mkoa wa Kilimanjaro, Rashid Omari amesema madereva Bajaj wamekuwa na changamoto kutokana na kukamatwa na askari hao.
“Japo wapo madereva wachache wanaovunja sheria lakini kuwakamata hata wale ambao hawajavunja sheria ni uonevu mkubwa. Kuna tabia ya baadhi mgambo hawa kuwaonea madereva hawa kwa makusudi,” amesema.
Amezitaka mamlaka husika kujadili na kutatua changamoto hiyo, zikiwamo faini wanazotozwa madereva hao akidai zinafika Sh100,000.