Serikali inatarajia kuongeza kilometa tano za ujenzi wa miundombinu ya mabasi yaendeyo haraka maarufu mwendokasi ambapo itaishia Vikindu,Wilaya ya Mkuranga, mkoani wa Pwani.
Sambamba na hilo pia kituo kikuu cha mabasi kwa mikoa ya Kusini kitaanzia hapo lengo likiwa kuwarahisishia wakazi wa mikoa hiyo usafiri.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa(TAMISEMI), Ummy Mwalimu leo Jumamosi Desemba 4,2021 katika uzinduzi wa ujenzi wa miundombiu awamu ya pili Mbagala Rangi Tatu.
Waziri Ummy amesema wameamua kutafsiri maoni, kiu na utendaji kazi kwa vitendo wa Rais Samia Suluhu Hassan wa kuwahudumia wananchi kwa vitendo na sio maneno kwa kuwasogezea usafiri huo wananchi.
“Kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha, Wizara ya Tamisemi na Wakala wa Mabasi Yaendayo Kasi (Dart) kuongeza kilometa tano kutoka Mbagala Rangi tatu hadi Vikindu, tunaamini Dart itafika mpaka Mkuranga Vikindu.
‘Lakini Mheshimiwa Rais ulituelekeza pia kwa sababu Mikoa ya Kusini hakuna kituo kikubwa cha mabasi,tunakusudia kujenga kituo kikubwa cha kutoka Kusini eneo ambalo miundombinu ya Dart itaishia ili kutoa huduma kwa mikoa hiyo,’amesema Waziri huyo.
Advertisement Akielezea kuhusu mradi huo wa Mbagala, amesema kukamilika kwake kutawezesha abiria 633,000 kusafirishwa kwa siku jijini Dar es Salaam na kutarajia kuingiza mabasi 755 barabarani kati yake 255 yatakua makubwa ya mita 18, mabasi 500 yenye ukubwa wa mita 12.
Pia ameeleza kuwa kutakuwepo na jumla ya ruti 30 kati ya hizo 11 zitakuwa za barabara kuu, 19.
‘Ukiachilia mbali hiyo, pia tumeshaweka kituo kikuu cha treni ya umeme (SGR) ili kufanikisha usafiri huo na ule wa mwendokasi,’amesema Waziri Ummy.