Dar/Mwanza. Baada ya miezi 28 ya kulitumikia Jeshi la Polisi mkoani Mwanza akiwa mkuu wake, Kamanda Ahmed Msangi amehamishiwa makao makuu ya jeshi hilo jijini Dar es Salaam.
Katika mabadiliko yaliyoyafanywa jana na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Simon Sirro kamanda huyo sasa anakuwa mkuu wa kitengo cha makosa dhidi ya binadamu makao makuu ya upelelezi Dar es Salaam.
Kamanda Msangi alihamishiwa mkoani Mwanza Aprili mwaka 2016 akichukua nafasi ya mtangulizi wake, Justus Kamugisha.
Viongozi hao walibadilishana vituo vya kazi kwa Msangi kuhamia Mwanza, huku Kamugisha akipelekwa mkoani Mbeya.
Taarifa iliyotolewa jana na Msemaji wa Jeshi la Polisi, Barnabas Mwakalukwa imesema nafasi ya Msangi imechukuliwa na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Jonathan Shana.
Wankyo Nyigesa, aliyekuwa mkuu wa operesheni kanda maalumu ya Dar es Salaam anajaza nafasi ya Shana Mkoa wa Pwani.
Mwakalukwa alisema mabadiliko hayo ni ya kawaida na yanatokea ndani Jeshi la Polisi katika kuongeza ufanisi kwenye utendaji kazi.