MKUU wa Mkoa wa Kagera, Brigedia Jeneral Marco Gaguti, ameongoza wakazi wa manispaa ya Bukoba na viunga vyake katika mapokezi ya Meli MV New Victoria iliyofanya safari yake ya kwanza kutoka Mwanza.
Akizungumza asubuhi ya leo na mwandishi habari hiikatika bandari ya Bukoba, amesema kuwa wakazi wa Mkoa wa Kagera wanapaswa kujivunia juhudi za Serikali baada ya kurejesha huduma za usafiri wa meli hiyo ambayo Serikali imetumia Tsh Bil 22.7 kuikarabati upya.
“Ujio wa meli hii unatarajiwa kuleta ajira zaidi ya 400 na kupunguza gharama za usafirishaji mizigo kutoka Mwanza na hata mikoa ya jirani inayotumia meli kupitia bandari za Mwanza na Bukoba.
“Awali tulikuwa na meli mbovu katika maziwa makuu, lakini sasa tuna meli zilizokarabatiwa na kufanywa upya zikiwemo New MV Victoria, MV Butiama na meli mpya ya MV Mwanza yenye uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 200 za mizigo,” alisema.
Meli hii ambayo zamani iliitwa MV Victoria sasa ni New Victoria Hapa Kazi Tu ambapo mara ya mwisho kutoa huduma katika Ziwa Victoria kati ya Mwanza na Bukoba ilikuwa Desemba, 2014 na ina uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 200 za mizigo.
Chanzo: Globalpublishers