Dar es Salaam. Watu watatu wamefariki dunia na mmoja kujeruhiwa baada ya lori kuacha njia na kuwagonga wakati wakiwa pembeni mwa barabara ya Sam Nujoma eneo la Mlimani City, jijini Dar es Salaam.
Ajali hiyo imetokea leo Jumamosi Novemba 23, 2019 saa 5:20 asubuhi. Lori hilo lilikuwa likitokea Ubungo kwenda Kijitonyama.
Akizungumza na Mwananchi Kamanda wa Polisi mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Mussa Taibu amesema ajali hiyo imetokana na uzembe wa dereva wa lori ambaye alikimbia baada ya ajali hiyo.
“Kati ya waliofariki mmoja ametambuliwa kuwa ni Daniel Mushi (20) mkazi wa Kimara Temboni, ni fundi umeme. Wengine bado hawajatambuliwa na miili yao imehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH),” amesema.
Amesema majeruhi anapatiwa matibabu hospitali, “gari linashikiliwa kwa kuwa dereva amekimbia. Tunaendelea na jitihada za kumtafuta lengo ni kuhakikisha anawajibishwa kwa mujibu wa sheria kwa sababu alichokifanya ni uzembe na kutozingatia sheria barabarani.”