Dar es salaam. Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimelaani kitendo cha baadhi ya polisi wa kituo cha Mburahati jijini Dar es Salaam kusambaza picha mnato za wanawake waliowakamata kwa makosa ya jinai.
Kauli hiyo imetolewa leo Ijumaa Julai 26, 2019 na Mkurugenzi mkuu wa LHRC, Anna Henga katika mkutano wake na waandishi wa habari, akibainisha kuwa katika picha hizo yaliwekwa maelezo ya makosa wanayodaiwa kutenda.
Henga amesema kufanya hivyo ni kinyume cha sheria kwa maelezo kuwa mahakama pekee ndiyo huweza kuthibitisha kama mtu ana hatia.
Akizungumza na Mwananchi kuhusu malalamiko hayo Kamanda wa Polisi Kinondoni, Mussa Taibu amesema kitendo si sahihi na kama walikamatwa walipaswa kupelekwa mahakamani kujibu mashtaka yanayowakabili.
“Sina uhakika na unachokisema nipe muda lakini sijui kulikuwa na sababu gani ya kuzirusha hizo picha kama waliwakamata walitakiwa kupelekwa Mahakama ya mwanzo kujibu mashtaka yao,” amesema Taibu.
“Ni marufuku wa mtu anayeshtakiwa kwa kosa la jinai kutendwa kama mtu mwenye kosa hilo mpaka itakapothibitika kuwa anayo hatia ya kutenda kosa. Tunalaani kitendo hicho na tunatoa wito kwa polisi kuchukua hatua za kinidhamu kwa waliofanya hivyo.”
Pia Soma
- Mahakama yapokea video kesi ya kina Mbowe
- Waliokutwa na nyama ya pundamilia jela miaka minne kila mmoja
- Maswali mengi hayajajibiwa makubaliano ya Barrick, Serikali