Dodoma. Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma, Godwin Kunambi amewataka viongozi wa Serikali za mitaa mjini Dodoma kutatua changamoto mbalimbali ikiwemo ya ujenzi holela wa nyumba.
Ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Novemba 28, 2019 mjini humo katika hafla ya kuwaapisha viongozi hao waliochaguliwa katika uchaguzi wa Serikali za mitaa uliofanyika Novemba 24, 2019.
Amesema maeneo yote ya Jiji la Dodoma yanatakiwa kujengwa kwa kufuata taratibu zinazotakiwa.
“Wananchi wanatakiwa kuwaripoti wanaoanza kujenga bila kufuata taratibu za ujenzi, viongozi wa serikali za mitaa simamieni wananchi wafuate sheria.”
“Mnatakiwa kutambua kila jambo linalotokea kwenye mtaa wako linakuhusu, iwe ni migogoro ya ardhi hatua ya kwanza ya kwako Kiongozi wa mtaa, ikitokea mwananchi ametoka kwenye mtaa na kupeleka tatizo lake ngazi ya juu ni wazi kuwa nafasi hiyo haikutoshi," amesema Kunambi.
Amewataka viongozi hao kutanguliza maslahi ya wananchi mbele ili kuwaletea maendeleo.
Msimamizi wa uchaguzi Jiji la Dodoma, Dickson Kimaro amesema katika uchaguzi wa Serikali za mitaa, CCM imeshinda kwa asilimia 100 katika mitaa yote 222.
Mwenyekiti wa mtaa wa Chinyonyo kata ya Kilimani, Faustina Bendera amewaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwake katika kutekeleza miradi mbalimbali .