Dar es Salaam. Wafanyabiashara wa Soko la Tandika wameiomba Serikali kutafuta namna ya kukusanya kodi ya zuio katika upangishaji ili kuwaondolea mzigo wa kulipa kodi ambazo zinapaswa kulipwa na wamiliki wa vibanda.
Hayo yalisemwa jana katika kufunga wiki ya elimu ya mlipakodi iliyosimamiwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Akizungumza na Mwananchi mfanyabiashara Hawa Abdul alisema asilimia 10 ya pango wanayotozwa na TRA, si halali kwao lakini ngumu kwa mmiliki kukubali kukatwa fedha hiyo katika kodi anayolipwa na mpangaji.
“Ni suala gumu mtu akupangishe halafu umwambie Sh150,000 ambayo ni asilimia 10 ya kodi yake unaipeleka TRA labda kama hutaki kufanya biashara,” alisema Hawa.
Naye Yusuph Mashaka alisema suala la kumkata mmiliki wake asilimia 10 liliwahi kumkosesha sehemu ya kufanyia biashara.
“Ilikuwa mtihani kila nikijitahidi kumwelewesha ilikuwa ngumu hadi akafikia kuniambia hataki niwe mpangaji wake,” alisema.
Pia Soma
- Wageni waonywa mifuko ya plastiki
- Membe amjibu Rostam urais mwaka 2020
- Mkindi: Kilimo bado hakijapewa hadhi ya kuwa uti wa mgongo
“Hii asilimia 10 ya kodi ya zuio katika upangishaji inatakiwa kulipwa na mmiliki wa nyumba baada ya kulipwa pango,” alisema.