WAWEKEZAJI kutoka India wanatarajia kuanza kujenga kiwanda cha kuchakata wanga kwenye zao la muhogo wilayani Handeni mkoani Tanga kwa gharama ya Sh bilioni 2.5.
Wawekezaji hao ni wa Kiwanda cha Lobo Agro Processing. Walisema hayo walipozungumza na Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Martine Shigela.
Walisema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho, unatarajia kuanza mwezi huu na kukamilika Juni mwaka huu.
Kiwanda hicho kitaanza kusindika zao la muhogo na baadaye mazao mengine
Mwekezaji, Inderjeet Singh Rehal alisema kuwa kiwanda watakachojenga kitakuwa na uwezo wa kuchakata mihogo tani 400 kwa siku moja, hivyo kumaliza changamoto ya soko kwa wakulima wilayani humo.
"Nia yetu ni kuzalisha wanga kwa ajili ya mahitaji ya soko la ndani na nje ya nchi kwani viwanda vingi vya vyakula vina uhitaji wa wanga kwa ajili ya kuhifadhi bidhaa wanazozalisha ili ziweze kudumu muda mrefu,"alisema Rehal.
Shigela alisema kuwa ujio wa wawekezaji hao ni moja ya jitahada za mkoa huo kumaliza changamoto za masoko kwa wakulima wa mazao mbalimbali.
Alisema walihamasisha wakulima walime zao la muhogo kwa wingi na waliitikia wito huo. “Tulikuwa na changamoto ya soko hivyo ujio wa kiwanda hicho ni mkombozi mkubwa kwa wakulima”alisema.