Arusha. Wanawake wanaochelewa kufanyiwa upasuaji katika Hospitali za Jiji la Arusha kutokana na wingi wao sasa mambo yatakuwa mazuri baada ya kituo cha afya cha Daraja Mbili kuanza kutoa huduma hiyo leo Jumanne Septemba 17, 2019.
Upasuaji wa kwanza katika kituo hicho umemalizika salama leo ikishuhudiwa mkazi wa Njiro, Susan Erick (27) akijifungua mtoto wa kike.
Mganga mkuu wa halmashauri ya Jiji la Arusha, Saimon Chacha amesema kuanza huduma ya upasuaji katika kituo hicho kilichofunguliwa mwaka 2017 ni faraja kwa wanawake.
Amebainisha kuwa kulikuwa na changamoto ya kutoa huduma kwa ajili ya wajawazito lakini kwa sasa ufumbuzi umepatikana.
"Leo watafanyiwa upasuaji wanawake wawili, mmoja ameshafanyiwa (Susan). Tunatarajia huduma hii itasogezwa katika kituo kingine cha Muriet ili kupunguza gharama za usafiri na kuepusha vifo vya wanawake,” amesema mganga huyo.
Dk Chacha amesema awali huduma za upasuaji zilikuwa zikifanyika Hospitali ya rufaa ya Mount Meru na St Elizabeth.
Pia Soma
- Watu 24 wauawa katika shambulio la kujitoa muhanga
- MWANANCHI JUKWAALA FIKRA: Mbinu hizi zitawawezesha wahitimu kujiajiri wenyewe
- Wanne wahukumiwa kunyongwa hadi kufa