Mkuu wa Wilaya ya Mafia, Mhandisi Martin Ntemo amesema ujenzi wa kituo ha afya katika eneo la kiegeani katika Wilaya hiyo unatarajia kuanza hivi karibuni.
Mhandisi Ntemo amesema kiasi cha Tsh.milioni 500 kilitolewa na Serikali kupitia mpango wa Malipo kwa Ufanisi (Results Based Finance – RBF) ambazo zitatumika kujenga jengo la wazazi, jengo kwa ajili ya upasuaji, nyumba mbili za watumishi na jengo la kufulia.
" Kupitia tozo ya simu, wilaya imepokea kiasi cha Sh.milioni 250 ambazo zitatumika kujengea jengo la wagonjwa wa nje (OPD), maabara na kichomea taka na tayari matofali 27,278 kati ya 40,000 yanayohitajika yamefyatuliwa" amesema
Ujenzi wa kituo hicho unaelezwa kuwa umeanza mwezi Oktoba na umepangwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi mitatu kwa gharama ya shilingi milioni 750.
Akizungumza na wananchi wa eneo hilo wakati wa uzinduzi wa ujenzi wa kituo na hicho Mhandisi Ntemo amewataka Vijana kujitokeza kushiriki katika kazi ambazo zimepangwa kutekelezwa kwa nguvu za wananchi.
Mkuu huyo wa Wilaya amesema amewahamasisha vijana kujitokeza zaidi kufanya kazi hizo pale inapohitajika mara kwa mara na kwamba kumekuwa na muitikio mdogo kwa kundi hilo huku wanaoonekana kujitokeza ni zaidi likiwa ni watu wenye umri mkubwa jambo ambalo halileti taswira nzuri kwa jamii.