Bunda. Watumishi wa umma nchini wametakiwa kuacha kutimia mitandao ya kijamii kurushiana vijembe badala yake watumie muda wao kuhudumia jamii kufikia lengo la Serikali la kupambana na umasikini.
Wito huo umetolewa leo Jumatano Mei 29, 2019 katika kijiji cha Hunyari halmashauri ya Wilaya ya Bunda vijijini na kiongozi wa mbio za mwenge kitaifa, Mzee Mkongea.
Mkongea alitoa kauli hiyo katika makabidhiano ya mwenge kutoka halmashauri ya Bunda mji kuelekea halmashauri ya wilaya ya Bunda vijijini.
Amebainisha kuwa kumekuwa na tabia ya baadhi ya watumishi hao kutupiana vijembe kupitia mitandao hiyo kila wanapokosolewa na wakuu wao wa idara.
“Unakuta mtu unakosolewa na mkurugenzi badala ya kutoa dukuduku lake hapo ili yaishe anakaa kimya na akitoka anakwenda kuweka maneno ya vijembe kwenye WhatsApp,” amesema Mkongea.
Amebainisha kuwa watumishi wa umma wana jukumu kuhakikisha wanamsaidia Rais John Magufuli kuwahudumia Watanzania, kwamba kuendeleza vijembe ni kutowatendea haki wananchi.