Dodoma. Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Patrobas Katambi ametoa agizo la kila kaya kupanda miti mitatu na atakayeshindwa kutekeleza agizo hilo atatoa Sh15,000 kwa kila mti ili kumlipa mtu wa kuupanda.
Katambi amewaambia waandishi wa habari leo kuwa Januari mwakani watafanya ukaguzi wa kuwabaini watakaokiuka agizo hilo, huku akisema lengo ni kupambana na upepo na vimbunga katika jiji la Dodoma.
“Kila familia inatakiwa kuwa na miti mitatu bila kujali kuwa ya matunda au ya kivuli na katika kuhakikisha kuwa hili linafanikiwa mamlaka husika zitafanya operesheni ili kuwabaini ambao hawatatekeleza.”
“Ukibainika hujatelekeza agizo hilo ni lazima utalipia Sh15,000 kwa mti mmoja na hiyo fedha itatumika kumlipa mtu ili kufanya shughuli hiyo. Tunataka kuifanya Dodoma kuwa ya kijani kupitia kampeni iliyozinduliwa na Makamu ya Rais, Samia Suluhu Hasani,” amesema Katambi.
Hata hivyo Katambi amesema kuwa kila shule ya msingi na sekondari inatakiwa kupanda miti 200, vyuo vya kati miti 500, vyuo vikuu miti 1000.
“Zipo taasisi ambazo nina mamlaka ya kuziagiza nazo zipande miti 100 kila taasisi lakini zipo ambazo sina mamlaka ya kuziagiza nitaziandikia barua ya kuziomba kutekeleza agizo hili,” amesema.
Katambi amesema kuwa watatafuta taasisi ambayo itahusika na upandaji wa miti pembezoni mwa barabara hivyo maeneo hayo yanatakiwa kutengwa na mamlaka za usimamizi wa barabara.