VIJANA wawili wamefariki dunia baada ya kuangukiwa kifusi cha udongo kwenye machimbo ya dhahabu katika Kijiji cha Ilindi Mwime mkoani Shinyanga.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga Debora Magiligimba alisema ajali hiyo ilitokea Februari 12 saa saa moja asubuhi katika shimo namba 11C, katika kata ya Zongomela wilayani Kahama.
Kamanda Magiligimba alisema watu hao walikuwa ndani ya shimo wakiendelea kutafuta dhahabu ndipo udongo ulipoanguka kwenye hilo na kuwafunika. Aliwataja marehemu hao kuwa ni Kija Walaga (25) na Msonga Giti (36).
“Chanzo cha vifo hivyo ni kuchimba dhahabu bila kuchukua tahadhali kwani shimo hilo lilikuwa halitumiki kwa muda kwa sababu ya matengenezo na mvua zinazoendelea kunyesha"alisema Magiligimba.
Kamanda Magiligimba alisema miili ya marehemu imehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya Kahama ikisubiri ndugu kwa taratibu za mazishi.
Alitoa mwito kwa wachimbaji wadogo wa dhahabu wazingatie taratibu na miongozo iliyowekwa na viongozi na kamati za madini kuhusu uchimbaji salama katika maeneo yao.