MIILI ya aliyekuwa Mbunge wa Ubungo na Waziri wa Kilimo katika Serikali ya Awamu ya Tatu, Charles Keenja na mkewe Cecilia Keenja, inatarajiwa kuagwa mkoani Dar es Salaam, keshokutwa.
Keenja na mkewe walifariki dunia Agosti 5,
mwaka huu wakati wakipata matibabu katika Hospitali ya Saifee, Dar es Salaam.
Keenja aliaga dunia alfajiri ya siku hiyo na mkewe alifariki dunia mchana.
Mdogo wa marehemu Clement Keenja, alisema jana kuwa, baada ya kuagwa, marehemu hao watasafirishwa kupelekwa Mamba Kisambo Moshi Vijijini na wanatarajiwa kuzikwa
Alhamisi.
“Wapendwa wetu wataagwa Jumatatu hii hapo Karimjee, itaanza ibada ya kuwaombea na kisha wananchi watapata wasaa wa kuaga wapendwa wao hao na kisha safari kuelekea Moshi itaanza,” alisema Clement kwa simu.
Alisema kwa sasa miili ya Keenja na mkewe imehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa
ya Muhimbili (MNH)- Upanga, Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Clement wanandoa hao wameacha watoto sita.
Keenja aliwahi kuwa Mkurugenzi wa Tume ya Jiji la Dar es Salaam mwaka 1996 hadi 2000.
Mwaka 2000 hadi 2005 alikuwa Mbunge wa Ubungo, Dar es Salaam na Waziri wa Kilimo na Chakula.