Arusha. Wafugaji wa jamii ya Kibarbeig wilayani Babati Mkoa wa Manyara wanatarajiwa kuanza kunufaika zaidi na utalii baada ya kuanzishwa vituo vya kuvutia watalii katika maeneo yao.
Akizungumza leo Jumamosi Julai 20, 2019 ofisa maendeleo ya jamii wa taasisi ya Chemchem Association, Walter Palangyo amesema wamejipanga kuboresha maisha ya kabila hilo kwa kunufaika na utalii.
Amesema jamii hiyo iliyopo katika kijiji cha Vilima vitatu, imewezeshwa kupitia vikundi vyao vya vikoba na itajengewa maboma ya utalii yatakayokuwa yakitembelewa na watalii watakaolipa fedha.
“Kuna kikundi cha Wicheda ba na Datoga vya jamii ya Kibarbeig ambavyo tumepatia Sh2.5 milioni ili kukuza mitaji yao na kuweza kufanya shughuli za ujasiriamali ikiwepo kuuza vitu vya asili kwa watalii,” amesema.
Kamishna wa uhifadhi wa mamlaka ya usimami wa wanyamapori (Tawa), Dk James Wakibara amesema jamii zilizopo eneo hilo la hifadhi ya jamii linaweza kunufaika na utalii kama wakizitumia fursa zilizopo.
"Mwaka jana hifadhi hii imeingiza zaidi ya Sh1.2 bilioni hivyo mnaweza kunufaika zaidi kama mkiendelea kuhifadhi eneo hili na kutumia fursa za utalii zilizopo,” amesema.
Pia Soma
- Mhasibu Arusha adaiwa kutafuna Sh85 milioni kila mwezi
- Sababu kuongezeka uzalishaji wa mazao Tanzania yatajwa
- Waziri aeleza wizi ukarabati reli Tanga-Kilimanjaro