Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Jokate Mwengelo amewataka viongozi wa halmashauri hiyo kutokwenda likizo na badala yake wahakikishe wanakamilisha ujenzi wa madarasa ili wanafunzi waliofaulu mtihani wa darasa la saba mwaka 2020 wapate kujiunga na kidato cha kwanza ifikapo Januari mwakani.
Jokate amebainisha hayo alipokwenda kukagua maendeleo ya ujenzi wa Shule ya Sekondari Wilaya ya Kisarawe, Janguo na Mloganzila zilizopo wilayani humo.
“Nimepita shule tatu zinazotekeleza miradi ya ujenzi wa madarasa kwa ajili ya kupokea wanafunzi mwakani na kama unavyojua mwaka huu Wilaya ya Kisarawe imefaulisha wanafunzi 2488 na ninataka hata mmoja asikose fursa ya kujiunga na masomo ya sekondari,” amesema Jokate.