Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Jamii iungane kupambana na ukatili kwa watoto

5ada68a5bcb3ce0799904e9b2b26db21 Jamii iungane kupambana na ukatili kwa watoto

Mon, 31 Aug 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

KATIKA gazeti hili kuna habari ya kusikitisha kuwa vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa watoto vimekithiti mkoani Morogoro.

Kwa mujibu wa Idara ya Ustawi wa Jamii mkoani humo, kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu, jumla ya matukio 2,848 ya ukatili yameripotiwa na kati ya hayo 1,287 walifanyiwa watoto na 1,561 walifanyiwa watu wazima.

Taarifa ya idara hiyo imesema matukio ya ukatili wa kijinsia yameongoza na kufuatiwa na ukatili wa kimwili matukio 699, ukatili wa kiuchumi matukio 551 na ukatili wa kingono matukio 111. Halmashauri ya Mji wa Ifakara inaongoza kwa kuripoti matukio ya ukatili 1,873.

Habari hizi ni za kusikitisha na zinaonesha kwamba katika jamii yetu ya Watanzania bado kuna watu wachache wanaofanya unyama huu kwa watoto na wanawake wasio na hatia.

Vitendo hivi vimeshamiri si kwa mkoa wa Morogoro tu, bali vimekuwa vikiripotiwa kila siku kutokea katika maeneo mbalimbali nchini.

Kibaya zaidi, inaelezwa vitendo hivi hasa ulawiti na ubakaji watoto, vinafanywa na watu wakaribu hasa ndugu wakiwamo wajomba, baba wadogo na wengineo.

Kushamiri kwa vitendo hivyo, kunaonesha kuna tatizo au kuna mahali tumekosea kama jamii, kiasi cha watu kujivika roho za kinyama dhidi ya watoto ambao tunapaswa kuwalinda.

Tukiwa sehemu ya jamii, tunatoa wito kwa jamii nzima kuunganisha nguvu ili kupambana na vitendo hivi vya kinyama na kuvimaliza kabisa nchini mwetu.

Pia tunatoa wito kwa serikali kuendelea kuwachukulia hatua kali za kisheria, wanaofanya ukatili kwa watoto hasa ubakaji na kulawiti ili iwe ni fundisho kwa watu wengine.

Tunatoa wito kwa jamii kuripoti matukio hayo katika vituo vya polisi; na pia iwe tayari kutoa ushirikiano na ushahidi mahakamani ili kuwatia hatiani watuhumiwa.

Vitendo hivi si tu vinadhalilisha utu wa mtoto, bali pia ni kinyume cha haki za binadamu na vinamchukiza Mwenyezi Mungu.

Chanzo: habarileo.co.tz