Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Jafo agoma kufunga machinjio, ataka yaboreshwe

Fb223c6d463f10b184a6ad643d373b95 Jafo agoma kufunga machinjio, ataka yaboreshwe

Wed, 5 Aug 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

WAZIRI wa Nchi, Ofi si ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Selemani Jafo amegoma kufunga machinjio ndogo na ameagiza Bodi ya Nyama Tanzania ihakikishe machinjio yote yanakuwa na ubora.

Alisema hayo jijini Dodoma wakati akifungua maonesho ya wakulima na wafugaji, Nanenane, Kanda ya Kati yanayofanyika katika viwanja vya Nzuguni. Jafo alisema wakati akitembelea mabanda alipata ombi afunge machinjio ndogo kwa kuwa kuna machinjio kubwa na za kisasa.

“Machinjio hayo madogo yakifungwa yataondoa ushindani katika biashara ya nyama nchini lakini yakiwapo yatakuwa na ushindani mkubwa na uchumi utaendelea kukua kwa kasi kubwa,” alisema.

Alisema, kuna fursa kubwa kwenye ufugaji wa samaki na kuwataka wadau kujitokeza kuwekeza pembeni mwa bahari na maziwa makubwa kwa kuweka vizimba ili kuchangia kuvunwa samaki kwa wingi kwa ajili ya matumizi hapa nchini na pia kuuza nje ya nchi.

Alisema kuna kila sababu ya kujitathimini kutokana na kuwepo kwa maarifa mengi ya kujifunza kilimo, ufugaji na uvuvi na kuzitendea haki fursa hizo. Alisema katika nchi mbalimbali watu walishindwa kufanya uzalishaji kutokana na nchi zao kuwa kwenye karantini kutokana na ugonjwa wa Covid-19, lakini Tanzania ilipata neema.

Pia alitaka matumizi ya mbegu bora kupewa kipaumbele na kupitia fursa ya kilimo lazima kusonga mbele kupitia tafiti.

“Serikali za mitaa zihakikishe maarifa yanafikishwa kwa wananchi ili yaongeze tija katika kilimo na uvuvi,” alisema.

Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk Rehema Nchimbi alisema maonesho ya Nanenane yamekuwa ni sehemu ya kujifunza na kujivunia.

“Kutokana na kujifunza kupitia maonesho ya Nanenane Singida si kame tena , hakuna njaa tena tumehama kwenye umasikini, njaa na ukame sasa tunastawisha mazao yanayotumia maji kwa ufanisi…tunatembea kwa ujasiri kifua mbele katika kuadhimisha ufanisi na mafanikio hayo kuna viashiria vizuri na Singida sasa ni wakulima wakubwa wa korosho na ni tishio,” alisema Dk Nchimbi.

Alisema Singida hivi sasa wanalima korosho, kuna ekari 25, 600 zimepandwa na sasa wanataka kuwekeza katika kilimo cha parachichi.

“Zinazaa wakati wowote katika mwaka zinahitaji maji tu, korosho za Singida zinazaa mara mbili kwa mwaka, mkorosho moja ukivunwa unatoa kilo 100,” alisema Dk Nchimbi.

Chanzo: habarileo.co.tz