Handeni. Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) limeanza ujenzi wa daraja la muda kurejesha mawasiliano kati ya Wilaya ya Handeni na Kilindi eneo la Nderema.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumanne Oktoba 29, 2019 meja Lenard Mpanga amesema ujenzi wa daraja hilo lililosombwa na maji ulianza saa 8 mchana, utakamilika ndani ya saa tatu.
Amebainisha kuwa wananchi wameonyesha ushirikiano katika ujenzi huo na kuwataka kutokuwa na wasiwasi kwa kuwa ujenzi huo utakamilika leo.
“Hii ni kazi ya saa tatu mpaka manne, changamoto ilikuwa ni kupata mawe ila viongozi wameshalifanyia kazi yamepatikana,” amesema meja Mpanga.
Kwa upande wake kapteni Msenye Nyahuga amesema wameshajenga kingo za daraja hilo, kinachoendelea ni kujaza mawe kisha kutandika daraja ili magari yaweze kupita.
Daraja hilo lilisombwa na maji Oktoba 25, 2019 kutokana na mvua kubwa kunyesha mkoani Tanga. Madaraja mengine yaliyoharibiwa na mvua hiyo ni Kideleko na Sindeni.