Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

JPM aahidi kuondoa kero ya maji Arusha

983b017ff47d0668beb7a248ebdefa2f JPM aahidi kuondoa kero ya maji Arusha

Sat, 24 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

MGOMBEA urais wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais John Magufuli amesema katika kipindi cha miaka mitano iliyopita serikali imetekeleza mradi mkubwa wa maji katika jiji la Arusha, unaogharimu Sh bilioni 520 na utakaozalisha lita milioni 160.

Amesisitiza kuwa serikali yake imedhamiria kuondoa kero ya maji katika jiji hilo maarufu kwa utalii

Aliyasema hayo jana kwenye mkutano wake wa kampeni, uliofanyika Uwanja wa Shehe Amri Abeid jijini Arusha, ambapo maelfu ya wananchi walijitokeza kumsikiliza pamoja na wagombea ubunge na udiwani wa CCM.

Alisema mahitaji ya maji ya jiji la Arusha ni lita milioni 106 na yanayozalishwa kwa sasa ni lita milioni 40.

Hivyo, mradi huo ukikamilika, uzalishaji wa maji katika Jiji la Arusha utakuwa lita milioni 200, hivyo kufanya kuwepo kwa ziada ya maji ya lita milioni 100.

Alisema serikali imefanya mambo mengi kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha, kwa mfano ujenzi wa hospitali nne za wilaya, vituo vya afya vinne na kukarabati vingine vinane, kununua mashine ya kisasa ya x-ray katika Hospitali ya Rufaa ya Mount Meru.

Pia serikali imetoa elimu bure, kujenga barabara za lami, kurejesha treni ya abiria na mizigo kutoka Dar es Salaam hadi Arusha, kujenga stendi kuu ya mabasi ya mkoa na miradi mingine mingi.

Aliahidi kuwa atakapochaguliwa tena kuwa Rais, serikali yake itajenga mazingira bora ya Watanzania kuwa matajiri.

Pia amesema atakuwa Rais wa Watanzania wote bila kubagua kwa misingi ya vyama, ukabila au udini.

“Nitakapochaguliwa tena kuwa Rais, naahidi nitakuwa mtumishi wa Watanzania wote bila kubagua vyama vyao, dini zao, makabila yao na ninamuomba Mungu anisaidie katika hili katika kutekeleza wajibu wangu.

“Tunataka kutengeneza mazingira ya watu kuwa matajiri, nataka niwahakikishie Watanzania wote, Tanzania ni tajiri, tembeeni kifua mbele,"alisema Rais Magufuli.

Rais Magufuli alisema Serikali ya CCM anayoiongoza, inajenga miundombinu ya barabara, maji, umeme, viwanja vya ndege, bandari, reli, huduma za afya zikiwemo hospitali za rufaa za kanda, mikoa, hospitali za wilaya, vituo vya afya na zahanati, kuweka mazingira bora ya uchimbaji madini na kuimarisha ulinzi na usalama ili Watanzania wawe na mazingira bora ya kufanya kazi na shughuli zingine za kiuchumi ili wawe matajiri.

Alisema kwa kutambua kuwa urais ni utumishi, hivyo wananchi watakapomchagua tena kuwa Rais katika kipindi cha miaka mitano ijayo, ataendelea kuwa mtumishi wao bila kuwabagua kwa misingi ya ukabila, udini, vyama au maeneo wanakotoka.

Kuhusu Mkoa wa Arusha, Rais Magufuli aliwaomba wananchi wawachague wabunge na madiwani wa CCM, kwani kwa upande wa Arusha Mjini alipata taabu sana kutekeleza miradi ya maendeleo kutokana na jimbo hilo kuwa chini ya upinzani. Alisema ilimbidi amtumie aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo, Mrisho Gambo kusimamia miradi ya maendeleo.

Kutokana na ugumu huo, alisema ndiyo maana alimruhusu Gambo kugombea ubunge katika jimbo la Arusha Mjini ili kwa kushirikiana na madiwani wa CCM watakaochaguliwa, waweze kusimamia miradi ambayo serikali inaifanya jimboni humo na mingine itakayokuja.

“Mwaka 2015 nilikuja kuwaomba kura, mlinipa mimi lakini mkaninyima mbunge na madiwani. Ukweli nilipata shida sana namna ya kufuatilia miradi hapa, ikanibidi nimuagize Gambo afanye kazi zake za Mkuu wa Mkoa lakini wakati huohuo afanye kazi kama mbunge wa Arusha Mjini,”alisema Rais Magufuli.

Alisema hakumfukuza Gambo Ukuu wa Mkoa, bali aliridhia akagombee ubunge baada ya Gambo kumuomba ruhusa.

“Sasa nawashangaa wanaosema simpendi Gambo, kama nilikuwa simpendi nisingerudisha jina lake, kwa hiyo wana Arusha kama mnataka maendeleo ya kweli, nileteeni Gambo,”alisema.

Katika mkutano huo, pia aliwaombea kura wagombea ubunge na udiwani wote wa CCM.

Chanzo: habarileo.co.tz