Dar es Salaam. Serikali ya Ireland imeipatia Tanzania Euro 1 milioni sawa na Sh2.5 bilioni kwa ajili ya kufanikisha mradi wa kuwakwamua vijana wa Mkoa wa Kigoma, hasa wasichana wanaopata mimba wakiwa na umri mdogo.
Mradi huo wa miaka minne unatekelezwa na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia idadi ya watu duniani (UNFPA) ukilenga kuwafikia vijana wa wilaya nne za Mkoa huo.
Balozi wa Ireland nchini Tanzania, Paul Sherlock amesema mradi huo wa ‘Ujana Wangu Nguvu Yangu’, unalenga kuwafikia vijana waliokatisha masomo, watapewa elimu kuhusu tabia hatarishi, mimba na ndoa za utotoni, ukatili wa kijinsia.
“Elimu ya afya ya uzazi, usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake ina mchango mkubwa katika maendeleo ya nchi. Hilo ndilo limetufanya tushirikiane na UNFPA katika utekelezaji wa mradi huu,” amesema.
Mwakilishi mkazi wa UNFPA, Jacqueline Mahon amesema shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha wanawasaidia vijana wa Kigoma licha ya ugumu wa maisha wanaopitia.
“Tunatambua Kigoma ni Mkoa wa pembezoni unaokabiliwa na changamoto lukuki na ndio maana UNFPA tunasema tutakuwa pamoja na vijana na kuhakikisha hakuna anayeachwa nyuma,” amesema Mahon.