Dar es Salaam. Watoto pacha, Brian na Brighton Gebo (3) waliopotea juzi Juni 21 huko Kivule, jijini hapa, walipatikana jana Juni 22, 2019 mchana katika Mtaa wa Mbondole ‘Kwa Mhaya’ walikookotwa na msamaria mwema.
Akizungumzia tukio hilo leo Juni 23, 2019 alipozungumza na Mwananchi, baba wa pacha hao, Gebo Gelasi amesema watoto wake walikuwa wanacheza nyumbani kwao, baadaye saa 5 asubuhi wakaanza kufuata ng’ombe waliopita karibu na nyumbani kwao mpaka huko Mbondole.
Amesema pacha hao wakiwa pamoja waliokotwa na mtu mmoja ambaye aliamua kuwapeleka kwenye msikiti wa Kwabigwa uliopo huko Msongola.
Amesema baada ya kufikishwa, Ustaadh wa msikiti huo aliyemtaja kwa jina moja la Fadhili, aliwahifadhi watoto hao wakati wakiendelea kuwatafuta wazazi wao.
“Tulitoa taarifa katika kituo cha polisi cha Msongola nao walitusaidia mpaka tukawapata watoto. Bahati nzuri Ustaadhi naye alitoa taarifa polisi, kwa hiyo ikawa rahisi kuwasiliana na kuwapata,” amesema Gelasi.