Rombo. Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Kilimanjaro, Patrick Boisafi ameipa siku tano halmashauri ya Wilaya ya Rombo kuhakikisha mafundi wanaojenga Hospitali ya Wilaya hiyo katika kijiji cha Kirongo wanalipwa fedha zao.
Pia, ametaka vifaa vya ujenzi kununuliwa ili waweze kukamilisha ujenzi kwa wakati.
Boisafi ametoa maelekezo hayo leo Jumatano Agosti 28, 2019 baada ya kutembelea Hospitali hiyo na mafundi kulalamikia kutolipwa mshahara tangu Mei 2019 hadi sasa.
Akiwa ameambatana na wajumbe wa kamati ya siasa Mkoa na Wilaya na watendaji wa Halmashauri, walikagua ujenzi huo ikiwa ni sehemu ya ukaguzi wa utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya CCM mwaka 2015-2020.
Amesema mafundi hao wamefanya kazi yao kwa umakini lakini hawajalipwa kwa sababu halmashauri haijatekeleza majukumu yake ipasavyo, kuitaka hadi Jumatatu Septemba 2, 2019 kulipa fedha hizo.
“Hamjatekeleza wajibu wenu, ninaomba niseme huu si utaratibu mzuri na hatuwezi kwenda kuzungumzia pembeni, fanyeni kazi mwalipe fedha zao kwa kuwa ni haki yao.”
Pia Soma
- Dk Bashiru asema vyuma vimekaza kwa wapiga dili
- Lukuvi asubiriwa kutangaza tathmini fidia ya kikongwe aliyedai ardhi kwa miaka 42
- Polisi yawakamata wanaodaiwa kuratibu maandamano kudai ndege ya Tanzania kuachiwa
Kaimu mhandisi wa Wilaya, Boniface Vedasto amesema uhaba wa saruji na mafundi kutolipwa ni moja ya changamoto inayokabili ujenzi huo.
Amesema walikubaliana mafundi hao walipwe fedha nusu ambayo ni Sh30 milioni, lakini bado hazijalipwa.