Arusha. Hali ya usafiri kutoka Kituo kikuu cha magari ya mikoani jijini Arusha imekua shwari licha ya ongezeko la abiria wanaokwenda maeneo tofauti.
Mwananchi limeshuhudia leo asubuhi Jumamosi Desemba 22, 2018 abiria wakiendelea na harakati za kukata tiketi huku wengine wakisubiri mabasi yanayoanzia safari zake mjini Moshi na Rombo kwenda maeneo ya Babati, Dodoma Singida, Igunga, Mwanza na Kahama.
Askari wa ukaguzi wa magari na askari kutoka kikosi cha usalama barabarani wapo katika kituo kikuu kuhakikisha sheria na kanuni za usalama zinazingatiwa.
Hata hivyo, idadi kubwa ya abiria ni wale wanaokwenda mkoa wa Kilimanjaro umbali wa takribani kilometa 72 kwa kutumia mabasi aina ya Coaster kwa gharama ya kati ya Sh2,500 hadi Sh3,000.
Baadhi ya abiria waliotaka kutumia usafiri wa mabasi ya safari za mbali ikiwemo ya Mwanza, Kahama na Bukoba kwaajili ya kushukia maeneo ya njiani hawaruhusiwi na wafanyakazi wa mabasi hayo.
"Hatuchukui abiria wanaoshuka maeneo ya karibu yakiwemo Magugu, Babati na Hanang tunataka abiria wanaokwenda Mwanza tu," amesema Ally Hassan