Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) wilayani Iringa, wametakiwa kupanga bei za maji zinazoendana na hali ya uchumi wa wananchi, ili kila mtanzania aweze kusogezewa huduma ya maji safi na salama nyumbani kwake.
Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi RUWASA, Mhandisi Ruth Koya akiwa katika ziara yake ya kikazi mkoani Iringa.
"Kumbukeni maji hayana mbadala na lengo la serikali ni kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma ya maji katika umbali usiozidi mita 400, hivyo uwepo wa miradi ya maji karibu na wananchi lazima uendane na gharama za kupata maji kwa kuzingatia hali ya kiuchumi ya wananchi- msipandishe bei hovyo kama soda," alisema Mhandisi Koya.
Mbali na bei, Mhandisi Koya aliiagiza RUWASA) wilayani humo kuhakikisha inasogeza huduma ya maji katika maeneo ya wafugaji kwa ajili yao na mifugo yao. -