Dodoma. Aliyekuwa ofisa elimu Sekondari Wilaya ya Chemba mkoani Dodoma, David Mwamalasa amesimamishwa kazi kwa muda wa wiki mbili kupisha uchunguzi wa matumizi mabaya ya Sh 259milioni.
Kwa sasa Mwamalasa amehamishiwa wilaya ya Chamwino kuendelea na majukumu mengine.
Fedha hizo zilitolewa na Serikali ya Tanzania kupitia ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali (Tamisemi) kwa ajili mradi wa P4R (Lipa kwa matokeo) kwenye shule za sekondari Mondo na Soya zilizopo wilayani Chemba mkoani hapa.
Shule ya Sekondari Mondo ilishika nafasi ya tisa katika kundi la shule 10 za mwisho katika matokeo ya mtihani wa kidato cha sita mwaka 2019.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Odunga, shule hiyo ilifungiwa mwaka jana kuchukua wanafunzi wa kidato cha tano na wakaguzi baada ya kubainika mapungufu katika miundombinu.
Akizungumza jana Jumanne Julai 16, 2019 katika mkutano wa hadhara shuleni hapo ambao uliwahusisha wanafunzi, walimu na wakazi wa kijiji cha Mondo, katika wilaya ya Chemba, naibu Waziri wa Tamisemi, Mwita Waitara alimwagiza Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Joseph Nyamuhanga kuunda timu ya uchunguzi itakayokwenda shuleni hapo kuchunguza tuhuma hizo.
Pia Soma
- Bobi Wine atangaza kuwania urais Uganda mwaka 2021
- Usaili JKT waibua tishio homa ya ini mkoani Mtwara
- TMDA yabaini dawa bandia sokoni
Waitara alimweleza Katibu Mkuu kuhakikisha mtumishi anayefanya kosa hahamishwi kwenda eneo jingine kwa nafasi yake ileile.
“Hatuwezi tukawa tunasambaza uozo, kama mtu amekosa achukuliwe hatua, kama ni kuwa demoted (kushushwa cheo) ama kufukuzwa kazi ili na wengine wajifunze wasifanye makosa yale yale, ”amesema.