FAMILIA 5,000 katika mji mkuu wa Juba zitapatiwa vifaa vya ufugaji nyuki na kutotolesha vifaranga kwa ajili ya kufuga kuku vilivyotolewa na Shirika la Maendeleo na Ushirikiano la Uturuki (Tika).
Vifaa hivyo vitatolewa kwa familia zenye maisha magumu ambazo zitapatiwa vifaa vya ufugaji nyuki na uvunaji asali zaidi ya 300 na viwili vya umeme jua vyenye uwezo wa kutotoa mayai 500 kila moja .
“Nina furaha kuwa hapa kutoa misaada itakayonufaisha familia 5,000,” alisema Balozi wa Uturuki nchini, Tugrul Biltekin katika hafla ya kukabidhi msaada huo.
Alisema ni muhimu kusaidia miradi ya ufugaji nyuki na kuku wakati huu nchi inakabiliwa na janga la ugonjwa wa covid-19 hasa kwa watu walio katika mazingira magumu ili waweza kujisaidia wenyewe kuliko kusubiri misaada ya chakula kutoka sehemu nyingine.
Naye, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Onyoti Adigo alisema mradi huo ni muhimu kwa wananchi kwani utasaidia kupata ajira na kuboresha maisha yao.
Naibu Mratibu wa Ofisi ya Tika Juba, Turgut Gazigil pia alikuwepo kwenye hafla hiyo.