Dodoma. Serikali ya Tanzania imesema ekari 150,000 zilizotengwa katika mto Rufiji zitatumika kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.
Naibu Waziri wa Kilimo, Omary Mgumba amesema hayo leo Ijumaa Septemba 13, 2019 wakati akijibu swali la nyongeza la mbunge wa Rufiji (CCM), Mohammed Mchengerwa.
“Eneo la ekari 150,000 zilizobakia zitatumika kufanya nini,”amehoji Mchengerwa.
Akijibu swali hilo Mgumba amesema Serikali imeagiza Tume ya Taifa ya umwagiliaji kuainisha maeneo hayo, kuona namna gani linavyoweza kutumika katika kilimo cha umwagiliaji.
Katika swali la msingi, Mchengerwa amesema katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 Serikali iliahidi kujenga kiwanda cha sukari katika jimbo la Rufiji.
Amesema hata hivyo ardhi iliyokusudiwa kujengwa kiwanda hicho kwa sasa amepewa mwekezaji ambaye hana nia ya kujenga kiwanda hicho.
Pia Soma
- Waziri asema TRA ina uhaba wa watumishi 2,249
- Jopo la madaktari kumjadili Askofu Ruwa’ichi leo
- Moto mkubwa wazuka Rombo, maduka tisa yateketea
- Familia yakubali Mugabe azikwe makaburi ya mashujaa
Akijibu swali hilo naibu Waziri Ofisi ya Rais (Tamisemi), Josephat Kandege amesema Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) ilipata mwekezaji kutoka Mauritius ambaye ni kampuni Rufiji Sugar Plant na kampuni ya Agro Forest Plantantions.
Amesema taratibu za kupata ardhi kwenye Serikali zote za vijiji na ngazi ya wilaya zilianza mwaka 2012 na kukamilika mwaka 2016.
“Nyaraka zote zimewasilishwa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambayo inaendelea na taratibu zake za kujiridhisha ili itoe hati,” amesema.