Dodoma. Halmashauri ya Jiji la Dodoma itatumia Sh950 milioni kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 37 yatakayotumika kukabiliana na upungufu wa vyumba vya madarasa uliodumu kwa miaka mitatu.
Akizungumza leo Jumanne Februari 19, 2019 katika ziara ya kutembelea miradi ya halmashauri hiyo, ofisa elimu wa Wilaya hiyo, Martine Mkwabi amesema mbali na kujenga vyumba hivyo, halmashauri hiyo itatumia Sh1.1bilioni kwa ajili ya ujenzi wa maabara.
“Watoto wote watakaochaguliwa kujiunga na masomo ya sekondari watapata madarasa. Katika kipindi cha miaka mitatu tutakuwa hatuna shida ya upungufu wa madarasa," amesema Mkwabi.
Wakati Mkwabi akieleza hayo, mwalimu wa Sekondari ya Miyuji, Fedilis Mjingi amesema amepokea Sh52 milioni kwa ajili ya ujenzi wa madarasa saba.
Amebainisha hadi Ijumaa, watakuwa wamekamilisha ili kuwawezesha wanafunzi waliokosa vyumba vya madarasa kuyatumia.
"Watoto wanasoma darasa moja wakiwa 60 au 55 tutawahamishia katika madarasa yatakayokamilika Ijumaa," amesema Mjingi.