Dodoma. Halmashauri ya Jiji la Dodoma kuanzisha mahakama ya Jiji itakayoshughulikia mashauri ya ukiukwaji wa sheria ndogo za jiji.
Hayo yameelezwa leo Jumamosi Novemba 30, 2019 na mkurugenzi wa Jiji hilo, Godwin Kunambi wakati wa upandaji miti eneo la Medelii kutekeleza agizo la makamu wa rais, Samia Suluhu Hassan.
Kunambi amesema halmashauri hiyo ipo katika mchakato wa kutengeneza sheria ndogo ili iwe lazima kila kaya kupanda mti katika eneo ilipo.
"Tumeanza mchakato wa kuandaa sheria ndogo ambayo itakuwa ni lazima kila kaya kupanda miti yoyote ile, itaamua yenyewe kama ya kivuli au matunda,” amesema.
Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Patrobas Katambi aliyemwakilisha mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk Banelith Mahenge amesema kuna desturi kupanda miti lakini hakuna utamaduni wa kuhakikisha inakuwa.
"Ili kuhakikisha kuwa miti hii inasimamiwa kila chuo kikuu kigawiwe miche 20,000 na wahakikishe inakuwa. Maeneo ya kupanda tutawaonyesha," amesema.