Moshi. Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Dk Tulia Ackson ameushauri uongozi wa Hifadhi ya Taifa ya Kilimanjaro (Kinapa) kutafuta namna ya kufikisha huduma ya maji katika kituo cha Kibo Hut ili kupunguza adha kwa kampuni zinazopandisha watalii Mlima Kilimanjaro.
Amesema mbali na kuweka maji katika eneo hilo pia kuna haja ya kuongezwa vyoo katika maeneo ya hifadhi ya mlima huo kwa madai kuwa vilivyopo ni vichache.
Tulia ametoa kauli hiyo jana Jumapili Agosti 4, 2019 baada ya kushuka mlima Kilimanjaro, ikiwa ni siku sita zimepita tangu alipopanda kwa ajili ya kuchangisha Sh100 milioni za kununua mashine za kutengeneza taulo za kike kupitia taasisi ya Tulia Trust.
Amesema kukosekana kwa huduma ya maji katika eneo hilo kunawapa wapagazi wakati mgumu wa kupanda mlima huo wakiwa wamebeba maji.
Amesema wakati akipanda mlima huo amekumbana na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na wapagazi kufanya kazini nyingi na kupewa malipo kidogo.
“Nimefika kilele cha mlima ila nimekutana na changamoto nyingi hasa kwa wapagazi kulipwa malipo kidogo na wengine kutopewa mavazi. Naomba Kinapa kushughulikia kampuni ambazo haziwalipi wapagazi pamoja na kuwawekea mazingira mazuri,” amesema.
Pia Soma
- Abiria wanusurika kuteketea kwa moto ndani ya daladala Dar
- Magufuli kuzindua maonyesho ya wafanyabiashara wa nchi 15 za SADC
- Utafiti sekta isiyo rasmi mbioni kufanyika nchini Tanzania
Mkurugenzi wa kampuni ya utalii ya Zara Tours, Rahma Adam amesema wamechangia dola 1,000 za Marekani kuiunga mkono Tulia Trust.