Musoma. Shida Masaba (55) ambaye ni dereva wa Mkuu wa Mkoa wa Mara, Adam Malima aliyelazwa katika hospitali ya mkoa wa Mara, hali yake bado haijatengema.
Dereva huyo alilazwa jana Jumapili Agosti 4, 2019 hospitalini hapo baada ya kupata mshituko kufuatia mwanaye, Kasobi kupata ajali akiwa anaendesha gari hilo.
Masaba ambaye amelazwa katika wodi ya grade, hivi sasa hawezi kuongea badala yake kila akimuona mtu anayemfahamu huishia kuangua kilio na kutamka maneno ya kujutia kitendo hicho huku akihofia hatma yake.
Kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya mkoa wa Mara, Dk Hosea Bisanda akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu Agosti 5, 2019 hospitalini hapo amesema kutokana na hali hiyo asingependa mgonjwa huyo kuhojiwa na vyombo vya habari.
Amesema ingawa dereva huyo hakuhusika katika ajali hiyo iliyotokea jana lakini alipata mshituko hali iliyosababisha kupata shinikizo kubwa la damu na kushindwa kupumua vizuri sanjari na kupata dalili za awali za ugonjwa wa kiharusi huku akiwa na maumivu makali kifuani hivyo kuhitaji muda mwingi wa mapumziko ili hali yake iweze kuimarika.
"Hata asubuhi amekuja katibu tawala wa mkoa hapa lakini ameshindwa kuongea chochote maana akimuona mtu yeyote anayemfahamu anailia huku akitamka maneno kama atapata wapi hela ya kulipa na kusema amefanya kazi ya udereva kwa zaidi ya miaka 15 bila kupata ajali lakini leo amekumbwa na janga kama hili," amesema Dk Bisanda
Pia Soma
- Mbunge hamasa ya uwekezaji wa Uingereza ziarani nchini
- Heche akwamisha kesi ya vigogo Chadema
- Rafiki wa Boby Wine afariki baada ya kutekwa
- Mauaji yanayoendelea Marekani, Rihanna amjibu Rais Trump
Soma zaidi: Gari la RC Mara lapata ajali likidaiwa kuendeshwa na mtoto wa dereva wake