Musoma. Mwili wa Kasobi Shida ambaye ni mtoto wa dereva wa Mkuu wa mkoa wa Mara, Shida Masaba (55) aliyefariki jana usiku Jumatatu Agosti 5,2019 katika Hospitali ya mkoa huo unatarajiwa kuzikwa kesho Jumatano katika makaburi ya Victoria, Manispaa ya Musoma.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumanne Agosti 6, 2019, mjomba wa marehemu James Makoye amesema maandalizi ya mazishi yanaendelea na wanatarajia mwili huo utazikwa saa nane mchana baada ya taratibu zote kukamilika.
Amesema baba wa marehemu, Shida aliyekuwa amelazwa katika hospitali ya mkoa wa Mara baada ya kupata mshituko kufuatia mwanaye kupata ajali akiwa anaendesha gari la Mkuu wa mkoa tayari ameruhusiwa kutoka hospitalini mchana wa leo.
Makoye amesema hali ya baba huyo pamoja na mke wake ambaye pia alizimia baada ya kijana wao kupata ajali zinaendelea vizuri ingawa ameomba wasihojiwe kwa maelezo bado wanahitaji utulivu wa hali ya juu.
"Sema tu una shida gani nitakujibu maana baba wa marehemu tayari ameruhusiwa yupo hapa nyumbani na mke wake pia yupo wanaendelea vizuri, tungependa tuwape muda kidogo wapumzike" amesema Makoye baada ya Mwananchi kuomba kufanya mahojiano na wazazi hao.
Amesema kulingana na taratibu wanatarajia mwili wa marehemu utachukuliwa kutoka katika chumba cha kuhifadhi maiti hospitali ya mkoa leo jioni ili uweze kulala nyumbani kwao Kigera kwaajili ya mazishi kesho.
Habari zinazohusiana na hii
- Alichokisema dada wa aliyefariki baada ya kupata ajali na gari ya RC
- Dereva wa gari ya RC iliyopata ajali analia kila mara
- Mtoto wa dereva wa RC aliyepata ajali afariki dunia
Mmoja wa wanafamilia ambaye hakutaka jina lake litajwe kwa maelezo kuwa yeye siyo msemaji wa familia amesema kuwa wamemshukuru Mungu kwa vile taarifa za msiba hazikuweza kuleta shida kwa baba wa marehemu huyo pamoja na mama yake
"Tunawapongeza madaktari kwa jinsi walivyoweza kumuandaa kisaikolojia baba wa marehemu maana sote tulikuwa tunawaza atazipokeaje taarifa za kifo maana hadi saa tano asubuhi alikuwa hajapewa taarifa lakini baada ya ushauri alipopewa taarifa aliomba kwenda mochwari kuuona mwili wa kijana wake na baadaye akaruhusiwa kuja nyumbani," amesema mwanafamilia huyo