Dar es Salaam. Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (Dawasa) kupitia mkoa wa kihuduma Ubungo imesema wananchi wa Kimara Golani wataanza kupata huduma ya maji hivi karibuni.
Taarifa iliyotolewa leo Alhamisi Agosti 15,2019 na Ofisi ya Uhusiano ya Dawasa imesema eneo hilo halina huduma ya maji safi kwa kipindi kirefu na mara utandazaji wa mabomba utakapokamilika itaondoa adha wanayokutana nayo wananchi.
Meneja wa Dawasa Mkoa wa Ubungo, Pascal Fumbuka amesema shughuli ya ulazaji wa mabomba ya usambazaji maji ya ukubwa tofauti ikiwemo inchi 2, 3, 4, 6, 8 na 9 kwa urefu wa kilomita 20 inaendelea.
“Eneo la Kimara Golani limekuwa na tatizo la huduma ya maji kwa kipindi kirefu hivyo kama Dawasa Ubungo tukaliweka katika maeneo ya utekelezaji kwa mwaka huu wa fedha ambapo mradi ukikamilika utaenda kuhudumia kaya takribani 4,000 katika eneo hili,” amesema Fumbuka.
Dawasa imesema inaendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya usambazaji maji katika maeneo tofauti ya Mkoa Dar es Salaam pamoja na baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Pwani ikiwa ni moja ya juhudi zakufikia asilimia 95 za upatikanaji wa maji ifikapo Desemba, 2020.