Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Dar kukosa maji kwa saa 16

Maji Mgao (600 X 365) Dar kukosa maji kwa saa 16

Fri, 14 Apr 2023 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira (Dawasa) imetangaza kuwa kutakuwa na kukosekana kwa huduma ya maji kwa wateja wanaotumia mtambo wa kuzalisha maji wa Ruvu Juu kwa wastani wa saa 16 siku ya Jumamosi.

Taarifa hiyo iliyotolewa leo Ijumaa, Aprili 14, 2023 na kitengo cha mawasiliano Dawasa, imeeleza kuwa katizo hilo la maji litaanza kesho saa 12 jioni hadi siku ya Jumapili saa 4 asubuhi.

“Sababu ni uruhusu matengenezo ya bomba kubwa la inchi 36 eneo la Visiga Saheni na kutoa matoleo mawili maeneo ya Kwembe na Msigani yanayolenga kuboresha upatikanaji wa huduma ya maji maeneo ya Kibamba Pangaboy na Mbezi Malamba Mawili,” imeeleza taarifa hiyo.

Imetaja maeneo yatakayoathirika kuwa ni pamoja na Chalinze, Chalinze Mboga, Msoga, Ruvu Darajani, Ruvu JKT, Vigwaza, Mlandizi, Mbwawa, Visiga, Maili 35, Misugusugu, Kongowe, Soga, Miembe Saba, Kwa Mfipa, Mwendapole, Tanita, Kwa Mathias na Kwa Mbonde.

Maeneo mengine ni Picha ya Ndege, Lulanzi, Kibaha, Kiluvya, Kibamba, Mloganzila, Mbezi Magari Saba, Mbezi Kwa Yusufu, Njeteni, Msigani, Kifuru, Mbezi Inn, Mbezi Stendi ya Magufuli, Mbezi Mshikamano, Mbezi Louis, Makabe, Msakuzi, Mbezi, Kimara,Tabata, Segerea, Kinyerezi, Kisukuru na Bonyokwa.

Pia wateja wa Kimara B, Kimara Korogwe, Bucha, Baruti, Ubungo, Magomeni, Ukonga, Uwanja wa Ndege, Kiwalani, Vingunguti, Gongo la Mboto, Pugu na Kisarawe watakumbwa na katizo hilo la maji.

Katizo hilo linakuja ikiwa ni miezi michache imepita tangu wakazi wa jiji la Dar es Salaam, wakumbane na adha ya mgao wa maji kutokana na bwawa hilo kukauka.

Oktoba 24, 2022 Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Amos Makalla alitangaza kuwepo kwa mgawo huo baada ya kutembelea vyanzo vya kuzalisha maji vya Ruvu Chini na Ruvu Juu na kujionea upungufu katika uzalishaji wa maji kulikosababishwa na ukame.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live