MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Dk Binilith Mahenge amezitaka taasisi zinazotoa huduma za kijamii mkoani humo zikiwamo TARURA, TANESCO na DUWASA kuandaa mpango kazi utakaonyesha ni namna gani watapeleka huduma za kijamii katika maeneo yaliyotengwa kwa ajili ya uwekezaji na makazi kwa lengo la kuvutia wawekezaji.
Dk Mahenge ameyasema hayo leo alipofanya ziara katika maeneo ya kiuwekezaji ya Nala,Nala IFM, Mahungu, Michese, Mkalama na Iyumbu mkoani humo.
Amesema wawekezaji wengi hawajitokezi kuwekeza katika maeneo yaliyotengwa kwa shughuli hizo kwa kuwa huduma za kijamii sio za kuridhisha.
“Wawekezaji wanasita kuja maeneo haya kwakuwa huduma nyingi za kijamii hamna jambo linalowapa hofu wakifanya uwekezaji shughuli zao nyingi zitakwama” amesema Dk Mahenge.
Aidha, Dk Mahenge amezitaka taasisi hizo kuhakikisha zinafanya kazi kwa kushirikiana ili kuhakikisha huduma hizo zinawafikia wananchi wakati mmoja na kuzitaka kutokuwa kikwazo kwa wananchi na wawekezaji kukosa huduma hizo muhimu.