Buchosa. Mkurugenzi wa Halmashauri ya Buchosa wilayani Sengerema Mkao wa Mwanza nchini Tanzania, Crispin Luanda amewatangazia kiama walimu ambao watakaobainika kujihusisha kimapenzi na wanafunzi watafutwa kazi.
Kauli hiyo imekuja siku chache baada ya Baraza la Madiwani la halmashauri hiyo kuagiza ofisi ya mkurugenzi kuwachukulia hatua walimu wenye tabia ya kujihusisha na mapenzi na wanafunzi wao.
Diwani wa Bulyaheke, Bageti Ngele alisema walimu wamekuwa na tabia ya kuacha kufundisha badala yake wamekuwa wakiwarubuni wanafunzi na kufanya nao mapenzi jambo ambalo halikubaliki.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumamosi Aprili 4,2020 Luanda amesema yeye na timu yake wamepanga kupita kila shule baada ya kufunguliwa kupiga kura ya vitendo hivyo ili kuwabaini walimu hao.
Vitendo vya walimu kujihusisha kimapenzi na wanafunzi kimekithiri wilayani Sengerema na kuleta kero miongoni mwa jamii ya maeneo hayo.
"Nimechoshwa kila mara halmashauri yangu kuandikwa magazetini juu ya tuhuma za walimu kujihusisha na mapenzi na wanafunzi, nimechoka kuchafuka, dawa ni kuwafuta kazi tu" amesema Luanda.
Pia Soma
- Makonda: Ukijifungia ndani kisa corona utakufa njaa
- Hoja ya Sugu matokeo urais Tanzania kupingwa mahakamani yawaibua wanasheria
- UCHAMBUZI: Wananchi wamepata chama mbadala cha siasa nchini?
Mmoja wa wanafunzi anayesoma shule ya Sekondari Nyakasungwa (jina limehifadhiwa) amesema walimu wamekuwa na tabia ya kuwarubuni ili kuwapasisha mitihani yao ya mihula.
"Mimi ni mmoja wa athirika wa suala hilo, linanitesa sana kwani mwalimu wangu amekuwa akinitaka kimapenzi na mimi nimekataa sasa imekuwa ni nongwa" amesema mwanafunzi huyo.
Mkuu wa Wilaya ya Sengerema, Emmanuel Kipole amesema walimu ni kioo cha jamii wanapaswa kuzingatia maadili ya kazi yao kuwasaidia wanafunzi na wawaone kama watoto wao.
Kipole amewatahadharisha walimu walio na tabia mbovu kuacha la sivyo watashughulikiwa.