Kakonko. Serikali wilayani Kakonko mkoani Kigoma nchini Tanzania imewataka baadhi ya wafanyabiashara wanaonunua mazao mbalimbali ikiwemo muhogo kuacha mara moja tabia ya kuwaibia wakulima wa zao hilo kwa kutumia upimaji wa lumbesa badala ya kutumia mizani halali ya upimaji.
Hayo yamebainishwa leo Jumamosi Septemba 14, 2019 na mkuu wa wilaya hiyo (DC), Kanali Hosea Ndagala wakati akifunga mafunzo ya awali ya kijeshi ya Jeshi la kujenga Taifa(JKT) kwa mujibu wa sheria katika kambi ya Kanembwa amesema serikali haitaweza kuwavumilia wafanyabiashara hao wanaorudisha nyuma uchumi wa wananchi hao.
Amesema ni marufuku kwa wafanyabiashara hao kutumia kipimo cha gunia katika ununuzi wa zao hilo ambapo ni kinyume na taratibu na kwamba wamekuwa wakichangia kushuka kwa thamani ya zao hilo.
Mwakilishi wa Mkuu wa JKT, Kanali Ahmed Abas amesema mafunzo wanayopata vijana hao wawapo kambini ni sehemu ya kuisaidia jamii katika malezi bora na yenye tija kwa vijana kutokana na uwepo wa utandawazi ambao kwa sehemu kubwa umekuwa ukiharibu maadili ya vijana wengi.
Kaimu Kamanda wa kikosi cha Kanembwa, Meja Alinani Siwingwa amesema zaidi ya vijana 1,000 wamehitimu mafunzo ya awali ya kijeshi kwa mujibu wa sheria JKT ambayo yamejumuisha mambo mbalimbali ikiwemo kilimo ambacho kimekuwa kikifanyika katika kambi hiyo.